Monday, April 13, 2009

Havitatajwa fedhaluka wala bilauri

Hakika kuna shimo wachimbako fedha, na mahali wapatapo dhahabu waisafishayo. Chuma hufunikwa katika ardhi,na shaba huyeyushwa katika mawe. Binadamu hukomesha giza;huyatafutatafuta hata mpaka ulio mbali, mawe ya giza kuu, giza tupu.

Hufikia shimo mbali na makao ya watu; palikosahaulika na nyayo zipitazo. Hining'inia mbali na watu, huyumba-yumba huko na huko. Katika ardhi ndimo kitokeamo chakula; na chini yake hupinduliwa kama kwa moto. Mawe yake ni mahali zipatikanapo yakuti; nayo ina mchanga wa dhahabu.

Njia ile hapana ndege mkali aijuaye, wala jicho la tai halijaiona. Wanyama wakali wajivunao hawajaikanyaga, wala simba mkali hajaipita. Huunyoshea mwamba wa gume gume mkono wake, huipindua milima hata misingi yake. Hukata mifereji kati ya majabali,Na jicho Lake huona kila kitu cha thamani. Hufunga vijito visichuruzike; na kitu kilichostirika hukifunua.

Bali hekima itapatikana wapi, mahali pa ufahamu ni wapi?

Mwanadamu hajui thamani yake, wala haionekani katika nchi ya walio hai.

Vilindi vyasema, "Haimo ndani yangu"
Na bahari yasema, "Haiko kwangu"

Haipatikani kwa dhahabu, wala fedha haitapimwa iwe thamani yake. Haiwezi kutiwa thamani kwa dhahabu ya Ofiri. Wala kwa shohamu ya thamani nyingi, wala kwa yakuti ya samawi.

Dhahabu na vioo haiwezi kulinganishwa nayo; wala kubadili kwake hakutakuwa kwa vyombo vya dhahabu safi. Havitatajwa fedhaluka wala bilauri; Naam Kima cha hekima chapita marijani. Yakuti ya rangi ya manjano ya kushi haitasawazishwa nayo, wala haitatiwa kima kwa dhahabu safi.

Basi hekima yatoka wapi? kwa kuwa imefichwa mbali na macho ya wote walio hai, na kusitirika na ndege wa angani. Uharibifu na mauti husema, "tumesikia habari zake kwa masikio yetu."

Mungu ndiye aijuaye njia yake, Naye ajua mahali pake. Maana anatazama hata miisho ya nchi, na kuona chini ya mbingu nzima. Apate kuufanyia upepo uzito wake; naam anayepima maji kwa kipimo. Hapo alipoiwekea mvua amri, na njia kwa umeme wa radi. Ndipo alipoiona na kuitangaza; aliidhibitisha, naam na kuichunguza.

Kisha, akamwambia mwanadamu: Tazama, kumcha Bwana ndiyo hekima. Na kujitenga na uovu ndio ufahamu