Monday, February 23, 2009

Mji wa zamani

Staftahi nikaimaliza  na mara tu nilopoamka kutoka, nilipigwa na uzito wa wazo ya kuwa nilikuwa nimekuja kujiburudisha. Basi nilijiarifu kimoyomoyo nisiwe na haraka kamwe, aghalabu, kawaida ni kama sheria. Ni kawaida ya waswahili kutokuwa na haraka haraka zozote. Sote tumeziskia kawaida zao zisizo kasi.  Utaratibu pasi harakati. Ni wanadamu wasiopenda kukimbia na nilijulishwa na boi mmoja kule ya kuwa sababu si joto jingi tu, bali mazoea tangu enzi.

Mhudumu yule aliponiona nimesimama dede, aliviringisha macho yake (ya kurembua). Ni kama kwayo alikuwa akinishangaa na kunionya ushamba wa bara niuwache kule. Isitoshe, nipo nchi ya pole, niende pole. "Unaondoka yakhe?" aliniuliza. "Naam" nilijikakamua kukisema kiswahili cha kuimba. "Aaah, kaka. Mbona hata chakula chenyewe hakijateremka?" . Nilitabasamu nakumpa ngano ya mkutano wa saa fulani, ambao nilishauchelewa. Aliniangalia juu chini kama kunipima na akijaribu kuficha kutoshawishika kwake, alinijibu "Haya basi, mapeni ni dala hamsini" huku akinipokeza cheti. Hamsa nikampa na kuuangalia mlango.

Jiji la mombasa si la kumpoteza yeyote, awe asiwe mgeni.  Moja kwa moja niliondoka kueleka mji wa zamani ambao kwa sababu ya ziara za watalii wengi, umebatizwa na kubatizika old town. Old town kwa jumla ni kijiji wastani chenye nyumba zinazo hesabu jadi na karne kuzidi. Niliashiriwa na kuelezwa historia ya majumba; ya kifahari na yasiyo yaliyosimama kijijini. Urembo wayo kwa kweli ulikiwa kwenye miaka yao. Kwa ujenzi stadi na ufundi usioaminika (majumba yenyewe ni ya mbao na ya horofa!!).  Kwa mpangilio unaozidi miji mingi  ya kisasa. Si rahisi amakweli kueleza uzuri wa kijiji hicho kikamilifu.Nina arifa moja tu:Maji usiyoyafika, hujui wingi wake.

ziwa, madafu na zaidi

Jiji ni la Mombasa... Safari yangu niliifunga toka Nairobi kuelekea  baada ya kukimaliza kibarua fulani katika shirika la Kenya ICT Board. Usiku wa safari ulikua ni mtulivu, mwanana hata; nami nilijawa bashasha mpwito. Tuliondoka saa nne kasorobo za usiku na kama kawaida, usinginzi ulinichukua mara tu nilipoingia kwenye basi, kuketi na kuuhisi ubembeo wa mwenendo. Nyweee....safari hiyo, na mara nilipozinduka, joto nisilolizoa lilitanda kote - hewa iliyojawa kijiharufu cha chumvi ikanijia, ndipo nikagundua nipo pwani.

Wakati huu, jua lilikuwa lishazuka. Mandhari ya pwani kama nilivyotaraji yalitawaliwa na minazi iliyoyumba kwa upepo mithili ya wachezaji stadi wanapovilegeza viungo katika ngoma, mbumbumbu haswa. Mawazo yangu yalinipeleka mbali sana, mwaka wa tisini na nane ambao ulikuwa ni mwaka wangu wa mwisho kulitembelea jiji hili.

Basi, kajifanya mwenyeji, nikatoka moja kwa moja kwenye kituo cha mabasi kuelekea jijini. Harufu nzuri ya kukaanga viazi, mihogo na mapocho tofauti ya uswahilini ilinijia na kunitosamo nisiweze kuupita mkahawa (nafikiri Mvita Hotel), uliokuwa bayana kwangu kama chanzo cha vizuri hivyo. Waswahili husema kama tamu inaua, basi na sumu kazi yake nini? Nilisalimu amri na kusema kweli, tamu yazo pocho pocho siisahau asilani.

Washikaji, hekaya zangu pwani (na zinginezo) basi ziangalieni papa hapa, nikikamilisha masalio ya siku hiyo, na za siku zilizofwatia. Mombasa, masalaala.......raha?!