Sunday, March 1, 2009

Dhamira badala

Kawaida ya waja ni ziendapo mawazo, hufwata kama bendera upepo. Nami nimesadiki, afua ni mbili - kufa na kupona. Aidha uende mbele au urudi nyuma, ufurahi au ujae simanzi...mifano i kote kote. Siku yangu ilinusurika kuharibika baada ya kuketi kwenye kiti kimoja cha umma. Basi akaja boi mmoja akaketi kando yangu. Sikufikiria lolote; si haki ya yeyote kujipumzisha hapa? 

Mara, kijana  akachomoa kibeti chake chenye mihela iliyopangwa kunyooka mithili ya askari gwarideni. Huku akiniangalia kwenye ncha la jicho, alianza kupiga binja. Nilipendua sura na kuangazia pengine. Kidogo, akakitia kibeti kwenye paja na kuanza kusema kiingereza cha puani. "Hello, hev you delivered the fen?", "no, no, no,no it need installed now!" majigambo ya wapwani? sikufahamu. Nakangazia pengine, wakati huu mbali zaidi. 

Ni kwa kasi za umeme jamaa yule alipogutuka na kuchomoka pale kitini.  Moja kwa moja alielekea asiangalie nyuma. Kibeti chake kikaanguka naye ameukaza mwendo. "Ali!" nikamuita jina la jumla ( na la heshima) aitwalo yeyote usiyemjua naye amezingatia kijia kana kwamba ardhi itafunga safari wakati wowote sasa. "Ali we!" hakupenduka bali aliendelea hadi kipeo cha macho, nisimuone tena. Kila mmoja aliyekuwa ameketi pale alijifanya ni kama hakuna lolote lililoendelea. 

Akomapo mwenyeji na mgeni koma. Nilisimama kwa utaratibu, na kutoka pale. Sikuwa nimeenda umbali wa sikio kusikia ndipo nikawasikia wale walioketi pale wakisema- mwerevu huyu po! angalinaswa na mtego na hakuwemo. Ni ujanja au ilikuwa ni kweli? nilijiuliza na kukinai, dhamira ya kusaidia wakati mwingine utaibadilisha.

No comments:

Post a Comment