Thursday, March 12, 2009

Taarab

Kwa wapenzi wa lugha, nimejivumbulia starehe iliyoswafi na tena yenye kuburudisha: TAARAB.

Kulingana na hadithi zinazoenea pwani hadi Zanzibari, muziki wenyewe  ulianzilishwa na Sultani Seyyid Barghash bin Said ambaye alijulikana kwa mapenzi yake ya maisha;  na kwa maisha yake ya raha  mstarehe. Alikisafirisha kikundi kimoja kutoka Misri ili waweze kumchezea taarabl-nyimbo zilizoimbwa kwa lugha ya kiarabu-kwenye Kasri lake Beit-al-Ajab (amakweli alikuwa mstarehe sultan!) .

Ladba umemsikia Siti Bint Saad? mwimbaji aliyevuma sifa Zanzi miaka ya nyuma. Siti, ambaye jina lake alipewa kwa kuwa dada taratibu sana, alijifunza uimbaji akiwa mchanga. Alianza na nyimbo za wakati wake, na kuendelea kujivumbulia utaratibu mpya hata kuzitafsiri nyimbo zenyewe kwa kiswahili. Dada hodari amekuwa changamoto kubwa kwa taarab tunavyoijua leo; mengineyo si ya dharura?

Kipindi cha Rusha Roho, ambacho hupeperushwa kila Jumapili kuanzia saa tisa kamili hadi saa moja za jioni, nilikigundua kibahati na sibu. Katika masafa ya mia moja na kitu nukta, radio citizen basi huwa ndio mpangilio. Nyimbo kama vile paka mapepe na nyinginezo (kumradhi nazijifunza bado!) hushauri, hukejeli, huelimisha na  huburudisha unono. Kuna dada fulani pia kwenye masafa tofauti wakati uo huo ambaye pia hupeperusha nyimbo za uswahilini fika. (Utafurahia umalenga stadi ulio kawaida ya nyimbo hizi)

Kiswahili chake Hasan, ambaye ndiye nahodha wa Rusha Roho pia ni cha kusisimua. Hata ukawa wewe mgeni tu, na kumsikiza ni kwa mara ya kwanza, utafurahia. Kipya kinyemi kisicho kidonda. Maneno yake huyachagua kwa ustadi  usiodhahiri, na pia ni jamaa mwenye raha tele; utapenda.

Sijui kama nimekushawishi fika? Kwangu mimi, tukitukuze kiswahili.

No comments:

Post a Comment